
Huu ni ushuhuda niliopewa na rafiki yangu wa muda mrefu ambaye tulikuwa tukiburudika sehemu mbalimbali za starehe. Ushuhuda huu alinipatia siku mbili baada ya tukio hilo kumkuta. Na mimi ningependa kukupatia mkasa huu ili upate kujifunza kupitia kisa hiki.
Tukio hilo lilikuwa hivi: Wakati tukiburudika majira ya jioni, siku ya Juma nne, katika baa moja, rafiki yangu aliokota kibeti (pochi/wallet) cha mtu asiyemfahamu na kukimbia nacho nje bila ya kunipatia taarifa. Alipotoka nje, alifungua kibeti hicho ili aangalie kuna nini? Alipofungua, alikuta kitita cha pesa na vitambulisho kadhaa vya mwenye kibeti hicho. Alipoona pesa hizo, aliamua kukimbia nazo hadi nyumbani kwake bila ya kunipatia taarifa/kuniomba ushauri.
Alipofika nyumbani kwake alichukua pesa hizo na kuzificha sehemu mbalimbali, ikiwemo kabatini, kitandani, sebuleni (kwenye masofa yake), na zingine kwenye nguo zake, akidhani kuwa njia hiyo itamsaidia dhidi ya pesa hizo zote kupotea kwa wakati mmoja.
Sasa baada ya muda kwenda (ilipofika usiku wa manane), maana ilikuwa ni usiku, akaona alale maana alitakiwa kwenda kazini kesho yake asubuhi. Wakati akiwa amelala, alisikia milio ya ajabu dirishani mwa chumba chake alipokuwa amelala. Alipoamka kwenda kuangalia milio hiyo ni ya nini, aliona paka mkubwa akitazama dirisha lake. Na kisha akaanza kuongea kwa kumwambia ampatie kile alichookota.
Kutokana na mshangao mkubwa alioupata, hakuweza hata kubisha, akachukua kibeti kile kisha akakusanya pesa zote alizokuwa ameficha sehemu mbalimbali za nyumba yake na kisha akampatia paka yule. Alipompatia hapo dirishani alienda kufungua mlango ili akamuombe msamaha paka yule kwa kile alichokifanya, lakini cha kushangaza alipotoka nje, hakuweza kumuona paka yule, kwani alikuwa ameshapotea.
Tukio lile lilimfanya akose usingizi usiku mzima na kulipopambazuka alishindwa hata kutoka nje ya nyumba yake. Na kuanzia siku ile, aliacha tabia ya kuchukua vitu visivyokuwa vya kwake.
Natumaini mkasa huu umeuelewa na kama una tabia hii utaacha mara moja, ili kukuepusha na matatizo mbalimbali.
Elimisha na Wengine!